Fahari ya Serengeti

Wednesday, January 18, 2017

APORWA MIFUGO BAADA YA KUACHANA NA UGANGA NA UNGARIBA

UKOO WAMPORA MIFUGO ALIYEAMUA KUOKOKA NA KUACHANA NA UNGARIBA,
“Wanadai ni adhabu ya kuachana na mila na desturi”
Serengeti Media Centre.
 Mkazi wa kijiji cha Wagete kata ya Rigicha wilayani Serengeti Mkoa wa Mara Goshiyi Maduhu(72)aliyeporwa mifugo baada ya kuokoka.
Picha na Serengeti Media Centre.

Mkazi wa kijiji cha Wagete kata ya Rigicha wilayani Serengeti Mkoa wa Mara Goshiyi Maduhu(72)ameporwa ng’ombe 3 na mmoja kuchinjwa na ndugu  kama adhabu baada ya kuokoka na kuachana na mila na desturi.
Uamzi wa mama huyo kuachana na kazi za uganga wa jadi na ungariba na kumrudia Mungu unadaiwa kuudhi jamii yake ya kabila la Wataturu kwa madai kuwa walikuwa wakimtegemea kwenye kazi za mila na desturi  na kukeketa watoto.
Afisa Mtendaji wa kata hiyo Musami Chimaja ,Mchungaji wa kanisa la AIC Wagete Abel Paulo na Polisi wilayani hapa wamethibitisha kutokea kwa matukio hayo januari 12 na 13 mwaka huu,na watuhumiwa watatu ambao ni ndugu zake Giseni Maduhu(62)Magarinja Gitambeka(30)na Gina Gitambeka (32)wote wakazi wa kijiji hicho wamekamatwa.
Afisa Mtendaji wa kata Chimaja alisema mara baada ya kupata taarifa za tukio la kupora ng’ombe mmoja januari 12 mwaka huu,alifuatilia na kukuta wameishamchinja na kuagiza warejeshe,hata hivyo badala ya kumlipa januari 13 walienda kuchukua ng’ombe wengine wawili kama adhabu ya kuwashitaki serikalini.
Akiongea na Serengeti  Goshiyi Maduhu alisema ,”nimefanya kazi ya uganga wa kienyeji na ungariba kwa muda mrefu,nikawa napata shida nyingi ikiwemo kuchanganyikiwa,nikaamua kumrudia Mungu,niliteketeza mikoba yote niliyokuwa  ili nizaliwe upya,”alisema.
Alisema uamzi huo wa kuokoa roho yake na kuepuka mkono wa serikali kwa mangariba uliudhi ukoo wake na kuanza kumfanyia vurugu,”kwenye kikao cha mambo ya mila na desturi wakaamuru nitoe ng’ombe kwa ajili ya matambiko,nikawaambia sihusiki na mila tena,wakaamua kuchukua kwa nguvu na kwenda kuchinja,”alisema.
Anna Masoya (51)mwanaye alisema baada ya kutoa taarifa ya kuporwa ng’ombe mmoja wakaamua kufuata wawili kwa nguvu huku wakidai wataendelea kuchukua mpaka ziishe ,”tuliamua kusimama kidete mimi na mama na kusaidiwa na mtendaji ili haki iweze kutendeka,maana mila za ukandamizaji hazipaswi kupewa nafasi,”alisema.
Mchungaji Abel Paulo alisema ,pamoja na kujitahidi kuwaeleza ndugu zake sababu za kuteketeza mikoba ya uganga,hawakumwelewa na kuahidi kuchukua mali zake kama adhabu ya kuachana na mila na desturi.
Polisi wilayani hapa wamethibitisha kukamatwa kwa watuhumiwa hao na kuwa uchunguzi ukikamilika watafikishwa kwenye vyombo vya sheria kujibu tuhuma zinazowakabili.
Mwisho.

0 comments:

Post a Comment