Fahari ya Serengeti

Tuesday, December 13, 2016

NGARIBA NGULI NA WENZAKE WAPANDISHWA KIZIMBANI,MMOJA AKIRI KUKEKETA MTOTO MMOJA

 Ngariba nguli Wansato Buruna(56)mkazi wa kijiji cha Rung'abure wilayani Serengeti kushoto aliyenaswa juzi usiku wa manane akitoka kukeketa watoto akiwa kizimbani katika mahakama ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wilaya ya Serengeti ,kulia ni ngariba Rhobi Marwa mkazi wa Machochwe pamoja na wenzao wanne akiwemo mzee wa mila Ryoba Magoiga wa kijiji cha Koreri wamefikishwa katika mahakam hiyo kwa makosa ya kuwafanyia ukatili watoto ,kuwakeketa kinyume cha Sheria.
 Wakiwa kizimbani


NGARIBA AKIRI KUKEKETA MTOTO MMOJA KATI YA WATATU ALIOSOMEWA SHITAKA.
Serengeti Media Centre
Ngariba mmoja kati ya watatu waliopandishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wilaya ya Serengeti Mkoa wa Mara amekiri kumkeketa mtoto mmoja badala ya watatu aliosomewa .
Mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa wilaya Ismael Ngaile Mwendesha mashitaka wa Jamhuri Jacobo Sanga akisoma hati ya mashitaka alisema Nyahoswe Mwita(34)ngariba na mkazi wa kijiji cha Burunga kata ya Uwanja wa ndege ,desemba 9 mwaka huu katika kijiji cha Burunga aliwakeketa watoto watatu wenye umri wa miaka (14) (16) wanafunzi wa Serengeti sekondari na mmoja wa miaka (12) mwanafunzi wa shule ya  msingi Burunga
Ngariba huyo Nyahoswe  aliyefikishwa mahakamani hapo pamoja na ngariba wengine wawili,mzee wa mila na msaidizi wa ngariba  waliokamatwa maeneo tofauti kwa makosa ya kukeketa watoto usiku  ,bila wasiwasi  alikiri kumkeketa mtoto mmoja,”nimesema mimi nilimkeketa …..peke yake si watatu kama mlivyosema,”alimtaja.
Kukiri kwa ngariba huyo kumkeketa mtoto mmoja ilimlazimu Hakimu Mkazi Mfawidhi wa wilaya hiyo Ismael Ngaile kuahirisha kesi hiyo ya jinai namba 233/2016 hadi desemba 14 mwaka huu,na  kwa watuhumiwa wengine katika kesi za jinai namba namba 234/2016, 235/2016  zikiahirishwa hadi desemba 16 kwa ajili ya maelezo ya awali.
 Mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa wilaya Ismael Ngaile mwendesha mashitaka aliwataja washitakiwa wengine umri na nafasi zao katika jamii  kwenye mabano kuwa ni Wasanto Buruna(56)(ngariba)mkazi wa kijiji cha Rung’abure,Bhoke Mseti(40)mkazi wa kijiji cha kitunguruma(msaidizi wa ngariba) ,Ryoba Magoiga(62)mkazi wa kijiji cha Koreri (Mzee wa mila)na Rhobi Marwa(56)(ngariba)mkazi wa kijiji cha Machochwe
Alisema washitakiwa katika maeneo na muda tofauti walikamatwa kwa makosa ya kuwafanyia ukatili watoto wa kike  kinyume na kifungu namba 169A cha sheria ya kanuni ya adhabu sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.
Akitoa ufafanuzi wa hati ya mashitaka kwa kila mmoja Mwendesha mashitaka huyo aliiambia Mahakama hiyo iliyokuwa imefurika wasikilizaji  kuwa  mshitakiwa Wasanto Buruna anakabiliwa na makosa zaidi ya matano,katika kosa la kwanza desemba 8 mwaka huu kwa kushirikiana na Bhoke Chacha waliwakeketa watoto wa kike wawili  wanafunzi wa shule ya Msingi Kitunguruma wenye umri wa miaka (13) kinyume cha Sheria.
Katika kosa la pili ,la tatu na la nne linalomkabili Wansato alisema desemba 8 mwaka huu aliwakeketa wanafunzi wawili wa shule ya msingi Kitarungu na katika kosa la tano desemba 10 mwaka huu akishirikiana na Ryoba Magoiga (mzee wa Mila) katika kijiji cha Koreri walimfanyia ukeketaji mtoto wa miaka (13)mwanafunzi wa shule ya Msingi Kambarage.
Akifafanua mashitaka yanayomkabili Rhobi Marwa ngariba kutoka Machochwe,alisema desemba 9 mwaka huu alimkeketa mtoto mwenye umri wa miaka (14)mwanafunzi wa darasa la sita shule ya msingi Kambarage na siku hiyo hiyo alimkeketa mtoto mwenye miaka (13) anayesoma shule ya Msingi Mbirikiri.
Mshitakiwa Ryoba Marwa (mzee wa mila)alipewa dhamana na Hakimu Anamaria Mushi ,huku washitakiwa wengine wakikosa dhamana kwa madai kuwa wakiachiwa wanaweza kwenda kuendelea kuwakeketa watoto ,hivyo watakaa mahabusu hadi desemba 16 mwaka huu wakati kesi yao itakaposomwa maelezo ya awali.
Katika hatua nyingine kesi inayowakabili Chacha Kiheta na mkewe Mugusuhi Chacha imeingia katika hatua nyingine baada ya kusomewa maelezo ya awali.
Mbele ya Hakimu mkazi mfawidhi wa wilaya Ismael Ngaile mwendesha mashitaka wa Jamhuri Jacobo Sanga akisoma maelezo ya awali alisema kuwa mnano desemba 21 ya mwaka 2015 washitakiwa walifanya ukatili dhidi ya watoto wao watatu wenye umri wa miaka 17,16 na 13.
Hata hivyo mara baada ya kusomewa maelezo hayo wote walikana na kesi kuahirishwa hadi desemba 16 mwaka huu ambapo jamhuri imekamilisha upelelezi na itawasilisha mashahidi wake,washitakiwa wamerudishwa mahabusu hadi tarehe hiyo.
Wazee wa mila na ngariba licha ya kupata mafunzo ya athari za ukeketaji kupitia Mradi wa Tokomeza Ukeketaji Serengeti unaotekelezwa na amref health africa tanzania na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu(LHRC) na kuapa mbele ya viongozi wa wilaya kuachana na kazi hiyo,wamebuni mbinu ya kuendesha ukeketaji usiku wa manane.
Mwisho.

 Wanashuka kwenye gari ili wapande kizimbani

 Wakielekea mahabusu baada ya kukosa dhamana hadi desemba 16 mwaka huu


 Ngariba Wansato akitoka mahakamani kuelekea mahabusu
 Anapanda gari la polisi tayari kwa kuanza safari ya kwenda mahabusu
Safari ya kwenda mahabusu

2 comments:

  1. Kaka hongera kwa kazi nzuri, naona kuna haja ya kuzidi kuipublish website yako ili watu waijue na waanze kuitembelea.

    ReplyDelete
  2. Na kwa kuwa Ukeketaji ni janga kubwana pengine la kitaifa, kuwepo na nguvu za ziada kuifanya blog hii ionwe na watanzania wote. Najua inawezekana.

    ReplyDelete