Fahari ya Serengeti

Wednesday, September 7, 2016

MTANDAO WA KUSAFIRISHA WASICHANA WANASWA

Mtuhumiwa wa mtandao wa kusafirisha wasichana wa kwanza kulia akiwa amekaa na baadhi ya wasichana aliokutwa nao.


ANASWA KWA BIASHARA YA KUSAFIRISHA WATU,
Serengeti Media Centre
Mkazi mmoja wa kijiji cha Masinki kata ya Ring’wani wilayani Serengeti Mkoa wa Mara anashikiliwa na jeshi la polisi kwa tuhuma za kusafirisha watoto kutoka wilaya ya Ngara Mkoa wa Kagera na kuwauza katika mikoa ya Mwanza na Mara.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara Ramadhani Ng’azi amelithibitisha kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo (Julitha Lucas 40)ambaye alikamatwa septemba 3 mwaka huu baada ya polisi kupata taarifa kutoka kwa wasamaria wema,huku akidai hilo ni tukio la kwanza kutokea mkoani hapo.
Hata hivyo inadaiwa wengine watatu hawajapatikana na haijulikani walikopelekwa ,huku kukiwa na taarifa kuwa wamekimbia baada ya kuambiwa kuwa wanakamatwa kuwa si raia na wanatakiwa kupelekwa kwenye makambi ya wakimbizi kwa madai kuwa si raia wa Tanzania.
Alisema mtuhumiwa alikutwa na wasichana sita ambao alikuwa amewaoza kwa watu mbalimbali na vijana wawili ambao walikuwa wameuzwa kwa watu wawachungie mifugo na miongoni mwao walibainika hawajui Kiswahili na wanadaiwa kuwa huenda ni raia wa Burundi.
“Wasichana hao wana umri kati ya miaka 15 hadi 18 na inadaiwa anawachukua kwao kwa madai kuwa wanakuja kufanya kazi za ndani,lakini wakifika huwaoza kwa gharama kuanzia sh 150,000 hadi 300,000 kwa kutegemea alivyo,na inasemekana wengine wako Mwanza ,Bunda na Serengeti,hapa tumemkamata na watoto 5 wa kike na wa kiume wawili,tunaendelea na uchunguzi ushahidi ukikamilika tutamfikisha mahakamani kwa makosa ya kusafirisha watoto,”alisema.
Wakiongea na waandishi wa habari watoto hao walisema mama huyo ambaye naye ni mzaliwa wa kijijini kwao humtumia wifi yake aliyeko kijijini hapo kumtafutia watoto kwa madai ya kufanya kazi ,lakini walipofika wakaishia kuozwa na wawili wamebainika kuwa na ujauzito tayari.
“Baada ya kufika siku ya kwanza tukaenda shambani ,kutokana nikakuta wamenunua vitenge na kuambiwa ninaolewa na kukabidhiwa mme ambaye hata sikuwahi kuzungumza naye,nikaenda nimekaa kwake kwa wiki moja akawa ananipiga sana na kunitishia kunikamata…niliporudi kwa mama huyo akasema mimi ni mkimbizi ninatakiwa kutulia na hata tukimpeleka polisi hatutamshinda si wazawa,”alisema mmoja wao huku akitokwa machozi.
Naye mtuhumiwa huyo alipoulizwa alikiri kuwa watoto hao aliwaleta yeye kwa ajili ya kuwatafutia kazi na baada ya kufika wakapata wanaume na kuwa fedha za mahari alipanga kuwatumia wazazi wake,na kuwa zaidi ya watoto 17 ameishawatoa kijijini na kuwauza maeneo mbalimbali.
(Lucas Nyanswi)ambaye aliozwa msichana aliyekuwa na mtoto mdogo kwa sh 100,000 alisema alitoa malipo ya awali kwa mama huyo akamfatia mwanamke,”kitanda hakizai haramu nilipewa na mtoto kwa mahari hiyo baada ya kuuza pamba,sikujua kama ni Mrundi lakini yeye alisema anawatoa Ngara,”alisema.
Mwenyekiti wa kitongoji cha Gwinyanki Gitiri Ikwabe alisema agosti 2 mwaka huu alifuatilia nyumbani kwa mama huyo na kukuta watoto 6 ambao alidai wamefika kumsalimia kwa kuwa alikuwa anaumwa,hata hivyo baada ya mwezi mmoja alifuatilia na kuambiwa wangeondoka septemba 2 mwaka huu.
Mratibu wa Kituo cha Nyumba Salama kinachohudumia watoto wanaofanyiwa ukatili Rhobi Samweli alisema walipewa taarifa na wasamaria wema kutoka kijijini hapo kuhusiana na mateso waliyokuwa wanafanyiwa watoto hao na kulazimika kutoa taarifa dawati la polisi la jinsia na baada ya kufuatilia ndipo wakabaini mtandao huo.
Idara ya uhamiaji wilayani hapa wanaendelea na uchunguzi ili kubaini uraia wa wasichana hao baada ya kuwepo wasiofahamu lugha ya Kiswahili na wanaongea lugha ambayo wenzao walidai kuwa ni watanzania.
Akutwa na wanyama wa ajabu.
Katika hali isiyokuwa ya kawaida mtuhumiwa huyo alikutwa amefunga wanyama wengi  wa ajabu ambao wanakijiji walishindwa kuwatambua,ambapo mwenyekiti wa kitongoji hicho Gitiri Ikwabe alisema pamoja na kufika nyumbani hapo mara kwa mara lakini hakujua kama anafuga wanyama hao.
Mwisho.









1 comment:

  1. Picha inasomwaje? Mtuhumiwa huyo yupo upande gani mwa picha hiyo kushoto au kulia.

    ReplyDelete