Fahari ya Serengeti

Thursday, December 17, 2015

LIGI DARAJA LA TATU SERENGETI YAKAMILIKA KWA TIMU YA KILIMA FC MABINGWA WILAYA








Mchuano mkali kati ya timu ya Kilima Fc na Kibeyo Fc fainali ya ligi daraja la nne ngazi ya wilaya ya Serengeti.


Kipa wa Kilima Fc akijiandaa kunyaka mpira kwa mbwembwe ,katika mchezo ambao Kilima iliibuka na ushindi mnono wa magoli 5-2 na kutawazwa mabingwa wa wilaya.


Apigwa chenga na kubaki chini huku mchezaji wa Kibeyo Fc akikota gozi kutafuta goli kama inavyoonekana hapo.

KILIMA FC MABINGWA WA WILAYA.
Serengeti:Halmashauri ya wilaya ya Serengeti Mkoa wa Mara imepanga kutenga bajeti kwa ajili ya michezo,itakayosaidia kuibua na kuendeleza vipaji kwa michezo mbalimbali.
Mbunge wa Jimbo hilo Mwalimu Marwa Ryoba alisema hayo jana wakati wa kuhitimisha mashindano ya ligi daraja la nne ngazi ya wilaya kwenye uwanja wa Sokoine,ambapo alisema wanadhamiria kufufua michezo ili waweze kutoa timu zenye ushindani katika maeneo mbalimbali.
“Mwakani naanzisha ligi yangu ambayo timu nitaziwezesha vifaa mbalimbali,hiyo itatusaidia kupata vijana wenye vipaji vizuri ili tuweze kutengeneza timu moja yenye ushindani,hata Mbeya City walianza taratibu chini ya halmashauri,”alisema.
Kwa upande Mkuu wa wilaya hiyo Mafutah Ally akikabidhi zawadi  iliyotolewa na Mbunge wa jimbo hilo kwa washindi watatu wa ligi hiyo iliyoshirikisha jumla ya timu nane kwenye vituo mbalimbali,alisema watazisaidia timu za Kilima Fc ya Natta mabingwa wa wilaya walipata sh 45,000, Seronga Fc walioshika nafasi ya pili (35,000)na Polisi Fc(20,000) yeye akitoa sh 50,000 kwa ajili ya waamzi wa mchezo huo.
“Mimi nategemea kuanzisha ligi kuanzia ngazi za kata kwa michezo mbalimbali,kama alivyosema mbunge tuweze kuibua vipaji kwa michezo mbalimbali ikiwemo ya wanawake,hayo yote ni kwa ajili ya kuwaweka vijana pamoja,kukuza vipaji na kuwafungulia fursa zingine kupitia michezo,”alisema.
Katika mchezo wa mwisho ulichezwa uwanja wa sokoine timu ya Kilima Fc ya Natta ilichukua ubingwa wa wilaya baada ya kuinyuka timu ya Kibeyo Fc kwa mabao 5-2,na kufanikiwa kupata sh 45,000 na kuwakilisha wilaya ligi daraja la tatu ngazi ya mkoa.
Kama walivyosema wahenga kutangulia si kufika ,Kibeyo kupitia kwa washambuliaji wake Marwa Julius na Kibisa walipachika mabao katika dakika ya 17 na 25 kipindi cha kwanza na kuwafanya Kilima kupoteana.
Hata hivyo katika dakika ya 28 mshambuliaji  wa Kilima Fc aliyeng’ara katika mchezo huo kutokana na kucheza mpira safi Sixtus Sabilo alifunga bao la kufutia machozi,na kufanya matokeo kuwa 2-1 kipindi cha kwanza.
Kipindi cha pili kila timu ilifanya mabadiliko ili kuimarisha kasi ya ushambuliaji na ulinzi,hata hivyo mshambuliaji Sabilo dakika 18 kipindi cha pili aliwanyanyua mashabiki baada ya kufunga goli zuri na kubadili sura ya mchezo,na kuwafanya Kibeyo kupoteana.
Dakika ya 20 mshambuliaji Samson Lucas alifunga goli la tatu baada ya kumzidi ujanja kipa wa Kibeyo,dakika ya 35 mshambuliaji Chisayama aliifungia Kilima goli la nne kwa kumvika kanzu kipa wa Kibeyo Mgabo,na dakika ya 44 Sixtus Sabilo alifunga kitabu cha magoli na kuibuka mfunga bora katika mchezo huo.
Katika mchezo wa awali timu ya Seronga iliyoibuka mshindi wa pili iliifunga timu ya Polisi kwa magoli 2-1,magoli ya Seronga yakifungwa na Paineto Yusuph na la Polisi likifungwa na Masaita Fulyas.
Makocha wa Kilima Fc Samwel Matete na Seronga Fc Erasto Joshua walisema wanajiandaa kwa ajili ya kufanya vizuri kwenye ligi daraja la tatu ngazi ya Mkoa na kuomba wadau mbalimbali kuzisaidia timu hizo kwa kuwa zinawakilisha wilaya.
Mwenyekiti wa chama cha Mpira wilaya Vedastus Makaranga alisema timu zilizoshiriki katika mashindano hayo ni pamoja na Itununu Fc,Mageta Fc,Kilima Fc,Kibeyo Fc,Motukeri Fc,Polisi Fc,Seronga Fc na Imara Fc.
Mwisho.

















Mbunge wa jimbo la Serengeti Mwalimu Marwa Ryoba akiwapongeza wachezaji wote kwa kushiriki ligi hiyo,na kuahidi kuanzisha ligi maalum ya kusaka vipaji atakayoifadhili mwenyewe,kulia ni mkuu wa wilaya Mafutah Ally
Dc Mafutah Ally akielezea umuhimu wa michezo kwa vijana na kuahidi kuanzisha michezo mbalimbali kwa makundi ya vijana wilayani humo na kabla ya sikukuu ya mpya mpya atashirikiana na wadau kuanzisha ligi maalum
Wachezaji wa timbu mbalimbali wakisikiliza hotuba za viongozi
Mkuu wa wilaya akikabidhi zawadi  ya sh 20,000 nahodha wa timu ya polisi Fc baada ya kushika nafasi ya tatu,
Nahodha wa timu ya Seronga ambayo imeshika nafasi ya pili itashiriki ligi daraja la tatu ngazi ya mkoa




0 comments:

Post a Comment