Fahari ya Serengeti

Wednesday, July 20, 2016

BAADHI YA HUDUMA ZA MATIBABU HOSPITALI TEULE YA NYERERE ZASITISHWA KUTOKANA NA TATIZO LA MAJI

 Baadhi ya wagonjwa na ndugu zao wakilalamikia mfumo mbovu wa hospitali kuwatoza fedha wakati wakijua baadhi ya huduma za matibabu zimesitishwa kwa ukosefu wa maji.

HUDUMA HOSPITALI ZASITISHWA KWA KUKOSA MAJI.
Serengeti:Baadhi ya huduma  katika hospitali Teule ya wilaya ya Nyerere wilayani hapa Mkoa wa Mara zimesitishwa kutokana na ukosefu wa maji hali ambayo kama haitatatuliwa mapema huenda akasababisha madhara makubwa kwa jamii.
Takribani miezi mitatu hospitali hiyo inayotegemewa na wakazi zaidi ya 200,000 wa wilaya hiyo na nje ya wilaya haina maji kutokana na kuharibika kwa pampu,hata hivyo baada ya matengenezo  hawajapata huduma ya maji kwa kile kinachodaiwa kuwa wanatakiwa kurekebisha miundo mbinu yao ya  bomba na tenki.
Wakiongea kwa kukata tamaa baadhi ya wanaoguza wagonjwa walisema wanalazimika kununua maji,kwenda na shuka zao kwa kuwa za hospitali ni chafu na hazifuliwi, na vyoo vya wagonjwa vimetapakaa  kinyesi kutokana na kutokuwa na maji.
“Nimefika hapa saa 3 asubuhi na mgonjwa wangu akiwa na hali mbaya,hadi saa 8 arasili hakuna huduma ,wauguzi na waganga wanasema hawawezi kutoa huduma wakati hakuna maji ,maabara na chumba cha upasuaji bila maji hawawezi kutoa huduma,”alisema kwa masikitiko Marwa Nyakibari.
Grace Joseph ambaye ana ndugu yake aliyelazwa chumba cha wazazi alisema,wanalazimika kununua maji mjini ,hata hivyo kwa wale wasiokuwa na uwezo wa kununua wanakabiliwa na hali mbaya zaidi.
Mganga Mkuu wa hospitali hiyo Emiliana Donald alidai kuwa huduma zinatolewa kama kawaida ,hata hivyo alikiri kutokuwa na maji kwa muda mrefu,huku akigoma kutoa ufafanuzi wa tatizo hilo ambalo linaweza kusababisha magonjwa ya mlipuko.
Meneja wa Mamlaka ya Maji Mugumu(Muguwasa)Mhandisi Dickson Gideon alisema kwa mjibu wa sheria ya Maji namba 12 ya mwaka 2009 wao wanawajibika kufikisha maji kwa mteja kupandisha kwenye tenki ni wajibu wake,hivyo kuitaka mamlaka iwapandishie maji hadi juu kwa gharama zile zile ni hasara na watashindwa uendeshaji.
“Pamoja na kuwa na hitilafu kwa sasa kwenye Control Panel baada ya marekebisho na kusababisha huduma kusimama ili isiungue tumeagiza vifaa na wakati wowote tutafunga,lakini hospitali lazima wabadilishe miundo mbinu yao ili maji yaende juu na hizo ni gharama zao si mamlaka,”alisisitiza.
Wakati mganga mkuu wa hospitali akidai huduma zinaendelea kama kawaida ,baadhi ya wauguzi na waganga waliokutwa wamekaa nje ya maeneo yao ya kazi walisema ,taarifa za uongozi wao hazina ukweli kwa kuwa hawatoi huduma katika mazingira hayo ambayo yanaweza kuwasababishia magonjwa ya mlipuko.
“Shuka hazifuliwi,hakuna maji maabara ,chumba cha wazazi ,upasuaji ,mawodini na vyoo vimetapakaa vinyesi harafu kiongozi anasema huduma zinaendelea,kama zinaendelea kwa nini wagonjwa wanalalamika kutopata huduma,?”walihoji baadhi ya wauguzi.
Boniphace Magori mkazi wa kijiji cha Remung’orori alisema alimfikisha mgonjwa wake akiwa na upungufu wa damu na kukuta hakuna huduma,na baada ya kuomba uongozi ndipo akasaidiwa .
“Kuna hatari ya kupata magonjwa ya mlipuko hapa maana hali ni chafu sana,tunatoka vijijini kuja kupata huduma kumbe tunakuja kubeba matatizo mengine,wagonjwa hawaogi ,hakuna maji kwenye vyoo ,”alisema.
Magreth John alisema wananunua dawa,kitanda wanalipia na maji pia ,ndani ya mawodi harufu ni mbaya hapakaliki kwa kuwa hata maji ya kufanyia usafi wauguzi wanawanyang’anya wagonjwa walionunua.
Hata hivyo kwa muda wa siku tatu sasa mji huo hauna huduma ya maji ya bomba hali ambayo inawalazimu wananchi kutafuta maji kwenye visima mbalimbali vya asili ambavyo si safi na salama.
Mwisho.

 Moja ya choo cha wagonjwa kikiwa kimetapakaa vinyesi kutokana na ukosefu wa maji hali ambayo ianweza kusababisha magonjwa ya mlipuko kama hatua za makusudi hazitachukuliwa kwa haraka.



1 comment:

  1. Poleni sana wana serengeti. maana hii ni hatari kwa afya za wagonjwa na hata wauguzi wenyewe, serikali ilione hili na kuchukua hatua za haraka.

    ReplyDelete