Fahari ya Serengeti

Wednesday, September 9, 2015

AJINYONGA KWA KAMBA BAADA YA KUKOSA NG’OMBE WA KULIPA MAHARI



Na Serengeti Media Centre
Mkazi wa kitongoji cha  Mihuru kijiji cha Kitarungu kata ya Nyansurura wilayani Serengeti Mkoa wa Mara amekufa baada ya kujinyonga kwa kamba ya katani ,chanzo kikitajwa  kukosa ng’ombe wa kulipa mahari.
Polisi wilayani hapa,uongozi wa kitongoji na serikali ya kijiji umethibitisha kutokea kwa tukio hilo kati ya septemba 7 na 8 majira ya usiku,ambapo Chacha Bruna(25)mwenyeji wa kijiji cha Nyabisaga wilayani Tarime ,alijinyonga kwa kamba ya katani hadi kufa.
Mwenyekiti wa serikali ya kijiji hicho  Yohana Gimano akiongea na Serengeti Media Centre kwa njia ya simu kutoka eneo la tukio ,alisema Bruna aliyekuwa amefikia kwa baba yake mdogo Diabe Marwa ,alifikia uamzi huo baada ya kunyang’anywa mwanamke kwa kushindwa kulipa mahari.
“ Yeye ni Mkazi wa Tarime lakini hapa kijijini  kuna ukoo wao,alipofika hapa alimtorosha binti mmoja(Rhobi Samweli)akakaa naye kwa muda wa siku nne,septemba 7 ndugu zake walifuata huyo binti ili atoe mahari,kufuatilia akaambiwa atoe ng’ombe 9,yeye akasema anaye mmoja….wakamfukuza mpaka atoe mahari ndipo apewe mke,usiku akaamua kujiua”alisema.
Alisema kuwa kabla ya kuchukua uamzi huo akiwa na kamba  ya katani alimwambia mwanamke mmoja kwenye mji aliokuwa anaishi,kuwa haoni faida ya kuishi na kuwa siku hiyo ndiyo mwisho wake,hata hivyo hawakufualia kwa kuwa hawakutegemea kama angechukua uamzi huo.
“Asubuhi wamekuta ananing’inia kwenye mti pembeni ya barabara akiwa ameishakufa…inaonekana alijinyonga usiku ule ule ,kwa kuwa wanadai hata chakula cha usiku hawakula naye,walijua yuko katika matembezi ya kawaida”alibainisha.
Naye Mwalimu Mkuu wa shule ya Msingi Kitarungu ambaye ni jilani yake alisema ,tukio hilo limebainika alfajiri wakati watu wanapita ,wakiwemo wanafunzi ,”suala la yeye kunyang’anywa mwanamke linajulikana ,na alionekana mwenye mawazo sana baada ya kushindwa kuelewana na ndugu wa mchumba wake,huenda ilimuathiri kisaikolojia na kukosa msaada wa ushauri”alisema.
Mmoja wa wahudumu wa baa iliyoko jilani na eneo la tukio ambaye hakutaka jina lake litajwe,alisema kuwa uhusiano wa Bruno na huyo binti ulikuwa wa muda mrefu ,”toka mwezi februari nilikuwa najua ni wachumba,na walikuwa wanawasiliana sana kwa simu,na  ilijulikana baadae baada ya kumtorosha na ndugu kufuatilia,”alisema.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara Philip Karangi hakuweza kupatikana kuzungumzia tukio hilo,hata hivyo Polisi wilayani hapa  wamesema uchunguzi wa tukio hilo  unaoshirikisha mganga  ili kubaini chanzo cha kifo hicho ukikamilika ndugu wataruhusiwa kuendelea na mazishi,na hakuna mtu anayeshikiliwa kuhusiana na tukio hilo.
Mwisho.

0 comments:

Post a Comment