Fahari ya Serengeti

Tuesday, February 10, 2015

MTUHUMIWA MMOJA WA USHIRIKINA AAGA DUNIA.




Ghati Kisiba (75 mkazi wa kitongoji cha Mereshi Kijiji cha Robanda wilayani Serengeti ambaye alikamatwa na kupigwa na wananchi kwa tuhuma za uchawi amefariki.

Serengeti:Mtuhumiwa mmoja kati ya wanne  waliokamatwa kwa matukio yanayodaiwa ya kishirikina katika kitongoji cha Mereshi kijiji cha Robanda wilaya ya Serengeti Mkoa wa Mara amefariki.
Kamanda wa polisi wilaya ya Serengeti Pius Mboko amemtaja aliyekufa kuwa ni Ghati Kisiba (75)mkazi wa kijiji cha Robanda,ambaye amefia   Teule ya wilaya ya Nyerere  alikopelekwa jana baada ya  hali yake kubadilika ,chanzo cha kifo chake kitajulikana baada ya uchunguzi  kufanyika.
Kamanda huyo alisema mtuhumiwa mwingine Chausiku Kyahama Mahiti(61)naye amepelekwa hospitali kwa ajili ya kupata matibabu ,”walipigwa na wananchi kabla ya kuwaokoa huko hivyo mmoja amepelekwa hospitali ili kupata matibabu kutokana na majeraha aliyopata”alisema kamanda.
Hata hivyo Mganga mkuu wa hospitali hiyo Kelvin Mwasha akiongea na Serengeti Media Centre kwa njia ya simu kuhusiana na tukio hilo  ,alisema Ghati alifikishwa hospitali akiwa amekufa hivyo hawakuweza kumtibu.
“Hakutibiwa hivyo hatuwezi kusema chanzo ni nini mpaka tufanye uchunguzi(post mortem) ndugu wa marehemu hawapendi kufanyika kwa uchunguzi kujua chanzo cha kifo…..katika hatua ya  kwanza tumebaini  mwili wake haukuwa na jeraha lolote.”alisema.
Alisema alifikishwa hospitali na ndugu zake wala si polisi kama ilivyodaiwa na kamanda wa polisi wilaya na baada ya kufika mapokezi na kubaini kuwa ameisha kufa walilipia gharama za kuhifadhi maiti.
Februari 7 majira ya saa 3.30 usiku mwaka huu Matiko Mkeya(20)anayefanya kazi ya kuchunga ng’ombe mali ya Stephen Nyamkinda alipotea ghafla akiwa ndani,na februari 8 msako ulianza kwa kushirikisha wakazi wa kitongoji cha Mereshi na hatimaye kijiji kizima cha Robanda.
Katika msako huo walifanikiwa kumkuta akiwa katika bafu la Chatu Mkali na Chausiku Mahiti  huku akiwa amefungwa sanda nyeupe yenye maandishi mekundu ya namba 7 , akiwa hajitambui,baada ya Chausiku kupigwa alikiri kuhusika na kumchukua kijana huyo kwa njia za kishirikina na kutaja mtandao wake.
Miongoni mwa mtandao wake ni marehemu Ghati Kisiba ,Wisaka Makuru(43)na Chatu Mkali,ambao walipigwa na nyumba 7 za watuhumiwa hao zikateketezwa kwa moto,na polisi wa kituo kidogo cha Robanda baada ya kuzidiwa waliomba msaada wa askari kutoka wilayani waliofanikiwa kuwachukua mikononi mwa wananchi waliokuwa wanataka kuwaua.
Hata hivyo baada ya kuchukuliwa kwa watuhumiwa waumini wa makanisa mbalimbali wakiongozwa na kanisa la EAGT anakosali Mkeya waliendesha maombi hadi fahamu zikamrudia,na kubainisha kuwa chanzo cha mkasa huo ni maziwa kwa kuwa mtuhumiwa Chausiku na mmewe Chatu Mkali walishindwa kulipa deni,ndipo wakaahidi kumshughulikia.
Wakiongea na hazeti hili watuhumiwa wakiwa polisi walisema kuwa walionewa,huku Chausiku akikiri kumtaja Ghati baada ya kuzidiwa na makosa na kuwa aliamua kumtaja tu,hata hivyo ilibainika kuwa walikuwa hawaelewani alimtaja kama njia ya kumkomoa.
Polisi wamesema wanaendelea na uchunguzi wa mkasa huo,huku wakikiri kuwa watuhumiwa hawawezi kuwaruhusu kurudi kijijini kwa kuwa wanaweza kuuawa.
Mwisho.

0 comments:

Post a Comment